Habari

WATUMISHI (NIRC) WATAKIWA KUFANYA KAZI KWA KUZINGATIA MAADILI NA UADILIFU.

WATUMISHI (NIRC) WATAKIWA KUFANYA KAZI KWA KUZINGATIA MAADILI NA UADILIFU.
Mar, 04 2024

SERIKALI imewataka watumishi Tume ya Taifa ya Umwagiliaji kufanya kazi kwa kuzingatia maadili na uadilifu ili kufanikisha azma ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwezesha sekta ya kilimo kuchangia asilimia 10 ya Pato la Taifa ifikapo mwaka 2030.

Hatua hiyo imeelezwa kuwa ndio chanzo cha serikali kuongeza bajeti ya Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC) kutoka bilioni 373.5 kwa mwaka huu wa fedha wa 2023/2024 kutoka shilingi bilioni 46.5 kwa mwaka 2021/2022.

Hayo yalibainishwa jijini hapa leo na Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu  Wizara ya Kilimo, Hilder Kinanga  alipomuwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Gerald Mweli katika ufunguzi wa Baraza la Wafanyakazi wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji.

Alisema ni muhimu watumishi Tume ya Taifa ya Umwagiliaji kufanya kazi kwa kuzingatia maadili na uadilifu ili kufanikisha azma ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kuwezesha sekta ya kilimo cha umwagiliaji  kuchangia asilimia 10 ya Pato la Taifa ifikapo mwaka 2030.

“Hatua ya ongezeko la bajeti hiyo inazingatia mahitaji halisi ya Tume na hivyo, Wizara ya Fedha kuongeza ukomo wa bajeti ya Tume hususan bajeti ya Matumizi Mengineyo kwa ajili ya uendeshaji wa ofisi zetu.  Nimefarijika kuhafamishwa kwamba eneo hili la ukomo mdogo wa bajeti ya Matumizi Mengineyo limekuwa likiboreshwa kila mara, mfano bajeti ya matumizi mengine imeongezeka kutoka ukomo wa Shilingi 885,184,000 mwaka 2020/2021 hadi Shilingi 1,638,184,000 mwaka 2021/2022 na Shilingi 4,796,882,000 mwaka 2023/2024.”alisema

Amesema lengo la serikali kuongeza bajeti katika sekta ya umwagiliaji ni kuhakikisha usalama wa chakula na kuongeza mchango wa umwagiliaji katika pato la Taifa.

Katika hatua nyingine Hilder alisema lengo la kuandaa baraza la wafanyakazi ni kuwaleta wahandisi pamoja kujadili na kuona namna gani wanaweza kufikia lengo la serikali la kufikia asilimia 10 ya mchango wa Sekta ya Kilimo katika pato la Taifa ifikapo mwaka 2030.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu Tume ya Taifa ya Umwagiliaji Bw. Raymond Mndolwa  alisema hadi kufikia Januari mwaka huu Tume inaendelea na utekelezaji wa miradi zaidi ya 54 ambayo imefikia asilimia 50 na itakamilika Juni mwaka huu.

Alisema kukamilika kwa miradi hiyo itawawezesha wananchi kuwa na kilimo cha umwagiliaji katika misimu yote ya mwaka na kutimiza lengo la serikali.

“Tunaendelea na uchimbaji wa visima na mabwawa katika maeneo mbalimbali nchini ili kufikia lengo kama tulivyoelekezwa na ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya kufikia ekari 1,200,000 za kilimo cha umwagiliaji ifikapo mwaka 2025,”alisema.  

Naye Katibu wa Baraza la Wafanyakazi wa NIRC Amina Mweta alisema balaza hilo la wafanyakazi litajadili mpango wa bajeti ya mwaka huu na kuweka mikakati ya utekelezaji wake lengo ni kusaidia  kuongeza ufanisi katika utendaji kazi na tija katika uzalishaji.

“Baraza la wafanyakazi ni muhimu hasa kwa kipindi hiki ambacho serikali inahitaji sekta ya kilimo ikue kwa asilimia 10 ifikapo mwaka 2030. Hivyo tunaendelea kusisitiza ushirikiano ili kuunga mkono jitihada za serikali katika kuinua kilimo nchini,”